
UTATU KATIKA BIBLIA
Kitabu hiki kinashughulika na masomo kama vile: Mgawnyiko wa imani kuhusu utatu wa Mungu; maandiko yatumikayo kufundishia utatu kimakosa; sura ya Mungu ni ya namna gani; tofauti ya kujifunua kwa Mungu katika Agano la kale na Agano jipya; maana ya majina matatu ya Mungu; majina ya Mungu katika Agano la kale na Agano jipya, n.k. Ni matumaini yangu kuwa utakuwa mwaminifu kufuatilia maandiko yaliyotumika katika masomo haya yote, bila kujali itikadi za kidini au imani.
Dibaji
Namshukuru sana Mungu kunipa nafasi hii muhimu ya kushirikisha ufunuo mwingine wa Maandiko matakatifu, kwa watu wote wanaopenda kusoma na kulielewa Neno la Mungu. Mimi nafikiri hii ni njia moja ya kuujenga mwili wa Kristo, ambao sisi ni viungo vya mwili huo. Kwa kawaida watu wanaopendana katika jamii, hupenda kushirikiana katika mambo yote yaliyo mema hata yaliyo mabaya pia.
Huduma yangu ya kufundisha Biblia kwa muda wa miaka zaidi ya ishirini, ikiwemo ya huduma mashuleni pamoja na chuo cha theolojia ya Biblia, imenipa uzoefu mkubwa wa kukutana na maswali kutoka kwa watu mbalimbali na itikadi mbalimbali; ambayo hayajibiki kwa kutumia majibu yanayotokana na imani za madhehebu. Lakini Biblia inapotumika kwa kujitegemea yenyewe na kanuni zake, bila kuingiza itikadi zetu, ina uwezo wa kujibu maswali yote kwa uthibitisho mkubwa!
Katika kitabu kingine kiitwacho “KANUNI ZA KUFASIRI BIBLIA” nilielezea kwa kirefu sana jinsi ilivyo muhimu kusoma Biblia kwa kutumia “KANUNI” zake. Kukosa kanuni hizo, kumesababisha kuwa na migongano mingi sana katika kuifasiri Biblia, na mwili wa Kristo kugawanyika kiimani hata kudharauliana sisi kwa sisi, kila mmoja akimhesabu mwenzake kuwa namepotoka kwa kunyosheana vidole. Imeonekana kuwa kutokana na hali, hakuna awezaye kumsaidia mwingine! Je, kanisa la Yesu litaendelea na mwendo mpaka lini?
Kwa mara nyingine tena, katika kitabu hiki kiitwacho, “UTATU KATIKA BIBLIA” nimekiandika kwa kusudi la kuwafahamisha watu wote, Biblia isemavyo kuhusu utatu wa Mungu, kwa kutumia KANUNI ZA KUFASIRI BIBLIA, ili kuweka wazi mambo ambayo yanafundishwa na kuaminiwa kwamba, yapo katika Biblia au la! Kuna mambo yanayotakiwa kusisitizwa lakini yanapuuzwa; na yale yasiyo na umuhimu yanasisitizwa sana!
Kitabu hiki kinashughulika na masomo kama vile: Mgawnyiko wa imani kuhusu utatu wa Mungu; maandiko yatumikayo kufundishia utatu kimakosa; sura ya Mungu ni ya namna gani; tofauti ya kujifunua kwa Mungu katika Agano la kale na Agano jipya; maana ya majina matatu ya Mungu; majina ya Mungu katika Agano la kale na Agano jipya, n.k.
Ni matumaini yangu kuwa utakuwa mwaminifu kufuatilia maandiko yaliyotumika katika masomo haya yote, bila kujali itikadi za kidini au imani. Mungu akubariki!